Advertisements

Tuesday, December 6, 2016

MAITI INAYOGOMBEWA SASA KUZIKWA DAR

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imeamuru mwili wa marehemu Ernest Materego uliosafirishwa Novemba 24, mwaka huu kwenda Bunda kwa maziko urejeshwe na kuzikwa Dar es Salaam.

Hukumu hiyo ilitolewa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba baada ya kusikiliza ushahidi wa mashahidi tisa wa pande mbili zilizokuwa zikibishaniwa wapi marehemu azikwe.

Materego alifariki Novemba 19, mwaka huu jijini Dar es Salaam na Novemba 24 mdogo wa marehemu, Gonche Materego aliyekuwa akimuuguza na wenzake walisafirisha mwili huo kwa ajili ya mazishi Bunda mkoani Mara.

Watoto wa marehemu, Joyce, Edwin, Rita, Irene na mama yao mzazi, Dinah Willige (65) walipinga mahakamani wakiomba mwili urejeshwe wazike Dar es Salaam kwa sababu wanadai baba yao aliwaambia akifariki azikwe Dar es Salaam.

Wadaiwa akiwamo mdogo wa marehemu, Gonche, mke mdogo wa marehemu, Mwajuma Hassani (39), rafiki wa marehemu Thobias Mwita (66) pamoja na  majirani walitaka mwili huo uzikwe Bunda wakidai kuwa marehemu alitaka kuzikwa kwao.


Akitoa hukumu, Hakimu Simba alisema hakuna ubishi kwamba Ernest alifariki dunia Novemba 19, hakuna ubishi Dinna alikuwa mkewe na walizaa watoto wanne.

“Hakuna ubishi kwamba marehemu Ernest alikuja Dar es Salaam tangu mwaka 1974, Hakuna ubishi kwamba Mwajuma Hassan alikuwa akiishi na marehemu kama mke na wamezaa mtoto mmoja, sitaki kwenda mbali zaidi kuhusu ndoa ya marehemu na Dinna wala ndoa ya marehemu na Mwajuma.

“Hoja iliyokuwepo mahakamani ni wapi mwili wa marehemu utazikwa, hii kesi haina uhusiano na mali za marehemu, Mwajuma na mdogo wa marehemu walimuuguza marehemu wakampeleka Hospitali ya Muhimbili ambako umauti ulimpata.

“Mdaiwa ni mdogo wake wa damu marehemu alikuwa na jukumu la kumuuguza kaka yake, hoja je ni sahihi kuzikwa Bunda.

“Kwa mazingira yaliyopo wadaiwa walichukua kwa nguvu mwili wa marehemu na kuupeleka Bunda, kufanya hivyo ni kosa na ni kinyume cha sheria, mwili ulitakiwa kuzikwa Dar es Salaam.

“Amri ya mahakama, wadaiwa wakabidhi kibali cha mazishi kwa wadai, mwili urejeshwe Dar es Salaam kwa ajili ya mazishi, gharama za kurejesha mwili Dar e salaam zitatolewa na wadai na kila upande utagharamia gharama za kesi,” alisema Hakimu Simba.

No comments: