Advertisements

Saturday, June 24, 2017

RBF- Kuondoka na Watendaji Wazembe

Serikali imesema haita wavumilia watendaji watakaoshindwa kusimamia ipasavyo mradi wa Malipo kwa Ufanisi katika kuboresha utoaji wa huduma za Afya “Results Based Finance” (RBF) ambao hivi sasa unatekelezwa katika mikoa minane hapa nchini.
Akifungua kikao kinacho wakutanisha Makatibu Tawala wa Mikoa, Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri, Wakurugenzi wa Halmashauri, Waganga Wakuu wa Mikoa na Wilaya, Maafisa Mipango kutoka mikoa inayotekeleza mradi wa RBF, Naibu Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mh. Seleman Jafo, amesema ni lazima kufanyike mabadiliko katika utoaji wa huduma za afya kuleta matokeo tarajiwa.
Naibu Waziri Jafo ametawataka Mameya na Wenyeviti wa Halmashauri kuhakikisha kuwa utekelezaji wa Mradi wa RBF unakuwa ni ajenda ya kudumu katika vikao vinavyofanyika kila mwezi ili kuwezesha kujua kiasi cha fedha zilizoletwa kwa ajili ya utekelezaji wa Mradi huo ili kuweza kuboresha huduma za afya kwa wananchi.
Katika hatua nyingine Waziri Jafo, ameiomba Benki ya Dunia ambayo ndiyo mfadhili wa mradi wa RBF kuangalia uwezekano wa kuwezesha utekelezaji wa Mradi wa huu kufanyika nchi nzima ili kuboresha utoaji wa huduma za afya nchini kote.
Naye Mwakilishi wa Benki ya Dunia Bibi Gayle Martine ameipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa hatua ambazo inazichukua katika kuhimiza suala zima la uwajibikaji na kusema kuwa hali hiyo imeongeza shauku ya Wadau wa Maendeleo kuendelea kuunga mkono jitihada zinazofanywa na serikali katika kuleta mabadiliko ya kiutendaji na utoaji wa huduma za jamii.
Akizungumza katika kikao hicho, Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Rais- TAMISEMI anayeshughulikia Afya Dkt. Zainab Chaula amesema ili kufikia malengo chanya yanayotarajiwa katika uboreshaji wa utoaji wa huduma za Afya kila mmoja katika eneo lake inabidi kutengeneza mpango kazi ambao ndio utakuwa dira ya utendaji kazi ili kuleta matokeo chanya.

Mradi wa Malipo kwa Ufanisi katika Kuboresha Huduma za Afya nchini Ulianza mwaka 2015 katika mkoa wa Shinyanga kama eneo la majaribio ambapo hadi hivi sasa unatekelezwa katika mikoa nane ambazo ni Mwanza, Shinyanga, Pwani, Simiyu, Geita, Kigoma, Tabora na Kagera.

No comments: