Advertisements

Wednesday, September 13, 2017

Leah Kihimbi: Tamasha la JAMAFEST limejaa vionjo mbalimbali vya Afrika Mashariki

 Mkurugenzi Idara ya Maendeleo ya Sanaa, Bibi Leah Kihimbi (kulia) akiangalia baadhi ya bidhaa toka kwa Wajasiriamali katika banda la Watanzania mjini Kampala wakati wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki (JAMAFEST) linaloendelea mjini Kampala nchini Uganda 13 Septemba, 2017.
 Mkurugenzi wa Sera na Mipango wa Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Bw. Petro Lyatuu akiangalia baadhi ya bidhaa toka kwa Wajasiriamali katika banda la Watanzania mjini Kampala wakati wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki (JAMAFEST) linaloendelea mjini Kampala nchini Uganda 13 Septemba, 2017.
 Mshiriki kutoka Jamhuri ya watu wa Burundi (kushoto) akiangalia moja ya nguo aliyoipenda katika moja ya mabanda ya Tanzania katika muendelezo wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki (JAMAFEST) linaloendeleo mjini Kampala, Uganda 13 Septemba, 2017.
Mhadhiri Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, Dkt. Mona Kalinga akiangalia moja ya nguo aliyoipenda katika moja ya mabanda ya Tanzania katika muendelezo wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki (JAMAFEST) linaloendeleo mjini Kampala, Uganda 13 Septemba, 2017. (PICHA ZOTE NA BENEDICT LIWENGA-WHUSM)

Na Benedict Liwenga-WHUSM, Kampala-Uganda.
Mkurugenzi wa Idara ya Maendeleo ya Sanaa, Bibi Leah Kihimbi amesema kwamba, Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki maarufu kama JAMAFEST limesheheni vionjo mbalimbali vinavyoelezea uhalisia wa utamaduni wa nchi Wanachama za Afrika Mashariki.

Kauli hiyo ameitoa leo mjini Kampala nchini Uganda katika muendelezo wa Tamasha hilo ambapo amefafanua kuwa, kupitia tamasha hilo washiriki kutoka Tanzania wamejifunza mambo mengi yakiwemo mavazi, vyakula na baadhi ya bidhaa ambazo baadhi ya nchi hazipatikani jambo ambalo amesisitiza kuwa, Viongozi waanzilishi wa tamasha hilo hawanabudi kuliendeleza kwakuwa linatoa fursa ya kuleta maendeleo na kukuza mahusiano.

“Idara ya Sanaa na Utamaduni sasa itakuwa na mkakati madhubuti ambao utajikita katika kupata vikundi bora mbalimbali kupitia mambo tuliyojifunza toka kwa wenzetu, lakini pia tunawashukuu sana wajasiriamali kwa kuleta bidhaa mbalimbali mbazo ni tofauti kwakuwa baadhi vimekuwa havipatikani sehemu nyingine, na pia kwa upande wa vikundi vya Tanzania nimeshuhudia moja ya kikundi cha Rwanda kikijifunza moja ya ngoma toka kwa kikundi chetu cha Tanzania hakika tamasha hili ni muhimu sana kwetu sisi na kwa wenzetu”, alisema Kihimbi.

Ameongeza kuwa, katika burudani zilizotolewa na baadhi ya nchi wanachama zimekuwa na vionjo adimu kama vile vichekesho, ngoma za kitamaduni pamoja na mavazi ya asili jambo ambalo limewavutia washiriki wengi huku akitoa msisitizo wa kutunza tamaduni za nchi wanachama kwa ajili ya maendeleo ya nchi hizo.

Kwa upande wake Mkufunzi wa Maigizo toka Taasisi ya Sanaa na Utamaduni (TaSUBA), Bibi, Christa Komba amesema kuwa, kwa upande wao wamekuja na igizo la ‘Mti’ ambalo maudhui yake yamejikita katika kusisitiza kuwa nchi wanachama wa Jumuiya ya Afrika Mashariki zinaungana kwa pamoja katika kufanya kazi pamoja kwa maendeleo ya pamoja hususani katika nyanja za sanaa na utamaduni.

“Maudhui ya igizo letu la mti ni kuonyesha kwamba hakuna mtu mwenye thamani kuliko mwingine kwakuwa yatupasa kufanya kazi kwa pamoja kwa maendeleo yetu kwa pamoja”. Alisem Bibi Christa.

Ameongeza kwamba, sanaa endapo ikitumika vema katika jamii yoyote ina nguvu katika mawasiliano na inasaidia kuboresha maendeleo ya jamii yoyote.

Tamasha la JAMAFEST lilianzishwa mwaka 2013 nchini Rwanda ambapo hufanyika kila baada ya miaka miwili baina ya nchi wanachama za Afrika Mashariki ambapo kaulimbiu ya tamasha hilo kwa mwaka huu inasema kwamba ‘Utamaduni na Ubunifu, Kiini cha Ajira na Umoja’.

No comments: