Advertisements

Sunday, December 17, 2017

WAHITIMU WA MAFUNZO YA MGAMBO GAIRO WATAKIWA KUISHI KIAPO CHAO CHA UTII KWA MATENDO


Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Mhe. Siriel Shaidi Mchembe ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo ya mgambo katika kata ya Rubeho akikagua gwaride.
Kamati ya Ulinzi na usalama ya wilaya.
Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Mhe. Siriel Shaidi Mchembe ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo ya mgambo katika kata ya Rubeho akiteta jambo na Mshauri Jeshi la Akiba Gairo, Major Balitoga (kushoto kwake) pembeni ni Diwani wa Kata ya Rubeho, Mhe. Mhe. Digwagwala (wa kwanza kulia).
Wananchi waliohudhuria hafla hiyo.
Mshauri Jeshi la Akiba Gairo, Major Balitoga akitoa machache mbele ya mgeni rasmi.
Diwani wa Kata ya Rubeho Mhe. Digwagwala akitoa shukrani zake za pekee kwa kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya kwa kuweza kuendesha mafunzo katika Kata yake.
Mkuu wa Wilaya ya Gairo, Mhe. Siriel Shaidi Mchembe ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya kufunga mafunzo ya mgambo katika kata ya Rubeho akikagua gwaride. Wahitimu wa Mafunzo ya Mgambo wakiwa katika gwaride la ukakamavu mbele ya mgeni rasmi.
Wahitimu wa Mafunzo ya Mgambo wakimsikiliza mgeni rasmi wakati akitoa hotuba yake.
Brass Bendi wakitumbuiza katika hafla hiyo ya kuhitimisha mafunzo ya mgambo yaliyofanyika katika kata ya Rubeho.
Wahitimu wa Mafunzo ya Mgambo wakipita mbele ya mgeni rasmi kwa gwaride la kutoa heshima. Na Kajunason/MMG. Mkuu wa wilaya ya Gairo, Siriel Shaidi Mchembe amewataka wahitimu wa mafunzo ya mgambo kukiishi kiapo cha utii kwa matendo na si maneno.

Hayo ameyazungumza leo Disemba 16, 2017 wakati wa hafla ya kuhitimisha mafunzo ya mgambo ambayo yalifanyika katika Kata ya Rubeho halmashauri ya wilaya ya Gairo ambapo mgeni rasmi aliwaasa wahitimu kutii yale yote waliyofundishwa ili kujenga uchumi wa Taifa.

Katika hotuba yake Mhe. Mchembe aliongeza kuwa mgambo wanapaswa kutumia elimu waliyoipata ili kuinua uchumi wao na jamii inayowazunguka bila kuwaonea au kuwatesa wananchi.

"Nawaombeni sana ndugu zangu mafunzo mliyoyapata ni muhimu sana katika taifa letu ni vyema sasa na nyie mkayaishi yale yote mliyofundishwa kwa kipindi cha miezi mitatu mliyoshiriki," alisema Mhe. Mchembe.

Aliongeza kuwa ni vyema mgambo wakawa mabalozi wema wa amani na si wao wawe mstari wa mbele katika vitendo vya rushwa, unyanyasaji wa wananchi na kuepuka kujihusisha kwenye uharifu kwa kukodisha magwanda yao.

Mhe. Mchembe aliwataka viongozi wa wilaya kufanya usaili tena kwa wale mgambo wote ambao wameshapitisha miaka 10 ili waweze kurudi kupata mafunzo zaidi.

"Kazi hii ya mgambo inahitaji kuendelea kujifunza mara kwa mara hivyo nawaomba viongozi wote fanyeni upya usaili wale wote ambao muda wa miaka 10 umepita warudie katika mafunzo waweze kuongeza ujuzi zaidi," alisema Mhe. Mchembe.

Alimalizia kwa kuwataka viongozi wa wilaya kuwahamasisha akinamama kujitokeza zaidi katika mafunzo ya mgambo maana idadi yao imeonekana kuwa ni ndogo sana ukilinganisha na wanaume ambao wao wamekuwa mstari wa mbele katika kujitokeza.

Mafunzo hayo ya miezi mitatu yalihitimishwa Disemba 13, 2017 yalisimamiwa na Mshauri Jeshi la Akiba Gairo, Major Balitoga kwa kushirikiana na Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ambapo jumla ya wahitimu 101 ambapo asilimia 11 tu walikuwa ni wanawake.

Wahudhuriaji hafla hiyo walikuwa ni Diwani wa Kata ya Rubeho Mhe. Digwagwala, Mtendaji wa Kata, Wenyeviti wa vijiji, viongozi wa dini, wazee maarufu na wananchi zaidi ya 200 walishiriki maadhimisho hayo.

No comments: