Advertisements

Friday, February 23, 2018

DC Mtanda Kuanzisha Wangabo Cup kupongeza juhudi za Wana Kirando.

Mkuu wa Wilaya ya Nkasi, Said Mtanda (jezi ya Njano) akiongea na baadhi ya wananchi waliojitokeza kushiriki Songambele ya Upanuzi wa Ujenzi wa Kituo cha Afya Kirando iliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mh. Joachim Wangabo (wa kwanza Kushoto).

Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mh. Joachim Wangabo amemtaka Mkuu wa Wilaya ya Nkasi Mh. Said Mtanda kuandaa tamasha la michezo ili kuwapongeza wananchi wa Kata ya Kirando kwa kujitokeza kwa wingi katika songambele ya ujenzi wa kituo cha Afya cha Kirando pamoja na ujenzi wa madarasa manne katika Shule ya Sekondari Kirando.

Ameyasema hayo baada ya kuona umati wa wananchi wa kata hiyo ulipojitokeza wake kwa waume kushambulia ujenzi wa msingi wa kituo cha afya cha kirando, ujenzi ambao unatarajiwa kumalizika baada ya miezi mitatu ukihusisha majengo manne ya maabara, mochwari, jengo la wazazi pamoja na wodi ya kinamama.

“Wanakirando Mmekuwa na mshikamano bila ya kujali Vyama vyenu na itikadi zenu…ninyi mnaongoza kwa kujitokeza katika songambele kuliko mahali kwengine popote, Mh. DC nakutaka unazishe tamasha la michezo ili kupongeza kwa hiki kilichotendeka hapa.” Rc Wangabo alisema.


Pamoja na hayo Mh. Wangabo aliahidi kutoa mipira ya miguu Minne, ya Netball miwili pamoja na Vikombe viwili vya mashindano hayo.

Kwa upande wake mkuu wa Wilaya ya Nkasi Mh. Said Mtanda baada ya kupokea maelekezo hayo alianzisha harambee kwaajili ya kuanzisha mashindano hayo na hatiame madiwani, na wajumbe wa kamati ya ulinzi na usalama ya Mkoa pamoja na Mkurugenzi wa halmashauri ya Wilaya Nkasi walichanga fedha na vifaa mbalimbali ili kufanikisha tamasha hilo ambalo Mkuu wa Wilaya alilipa jina la Wangabo Cup.  

No comments: